Mto Kiwira unazidi kupanda chati kuliko mito mingine wilayani humo kutokana na kuwapo kwa Daraja la Mungu.
Image result for daraja la mungu
Lakini pia karibu na daraja hilo yapo maajabu mengine yakiwamo ya chekeche la uchafu unaokusanywa na maji  kabla ya kuingia eneo maarufu la Kijungu.
Kijungu nayo ni sehemu ya Mto Kiwira, ni eneo la ajabu kwa sababu mwamba wake umeumba kitu kama chungu kinachopokea maji yote na kuyapeleka chini bila kupitisha juu ya mwamba.
Inaelezwa kwamba mtu anayetaka kuvuka salama kwenye mwamba juu ya Kijungu kutoka upande wa Mashariki lazima atumie mguu mmoja wa kulia na akitokea Magharibi atumie mguu wa kushoto tu ili asitumbukie.
Maajabu mengine ni kuwapo kwa taarifa zinazodai mtu akizama kwenye mto huo, lazima afuatwe mzamiaji mmoja aliyerithi kazi hiyo kutoka kwa aliyekuwa kiongozi wa kimila na kwamba bila huyo,  aliyezama hawezi kuonekana mpaka siku saba zitakapopita.
Lakini jambo kubwa linaloonekana na kustaajabisha ni  kuwapo kwa daraja linaloaminiwa na wakazi wa eneo hilo na wilaya nzima ya Rungwe kwamba lilitengenezwa na Mungu  kwenye eneo la  Mto Kiwira unapotenganisha Vijiji vya Lugombo kwa upande wa Mashariki mwa mto huo na kile cha Mboyo  kilichopo Magharibi.
Mto Kiwira ni mojawapo ya mito minne inayotoka Mlima Rungwe  kupeleka maji kwenye Ziwa Nyasa. Mito mingine inayopeleka maji kwenye Ziwa Nyasa ni Lufilyo, Mbaka na Songwe, lakini kila mto una sifa za maajabu  yanayotofautiana.
Mto Kiwira unatofautiana na mito mingine kwa mambo mengi yakiwamo ya kuwa mto wenye urefu wa karibu kilometa 70 kutoka chanzo chake kilichopo Mlima Rungwe hadi Ziwa Nyasa na pia upo chini ya ardhi kwa umbali wa karibu kilometa mbili kutoka usawa wa Mji wa Tukuyu  ambao ni makao makuu ya wilaya hiyo.
Mto Kiwira umepewa jina hilo kutokana na matawi mengi ya mto huo kupitia karibu na Mji Mdogo wa Kiwira ambao ni maarufu kwa kuuza matunda mbalimbali kwa bei poa  wilayani Rungwe.
Sehemu kubwa ya maji ya mto huo yanaonekana kuwa meupe kutokana na kuwapo kwa maporomoko madogo madogo mengi yanayopitisha maji kwa kasi inayokadiriwa kuwa kilometa 50 kwa saa.
Lakini pia yapo mabwawa ya mto huo yaliyotuama kiasi cha watu wegi kujiuliza kama maji yamesimama ama yanaendelea mbele.
Kwa upande mwingine, mto huo pia unafanya kazi moja ya kiserikali ya kugawa mpaka wa vijiji katika Wilaya ya Rungwe, na pia unagawa mpaka wa Wilaya za Rungwe na Ileje, Kyela na Ileje kabla ya kuingia Ziwa Nyasa.
Umbile  la Daraja la Mungu
Kama ilivyodokezwa hapo juu, Mto Kiwira upo chini zaidi ya ardhi ya Wilaya ya Rungwe na una maajabu mengi, lakini moja wapo ni la kuwapo kwa daraja linaloaminiwa kuwa la Mungu linaunganisha vijiji vya Lugombo na Mboyo Kata ya Lufingo , wilayani Rungwe.
Daraja hilo limeundwa kwa mwamba wa mawe ukiwa na urefu wa karibu mita 12 na upana wa wastani wa mita tatu.
Kwa mujibu wa kijana Christopher Suleiman ambaye ni mwongozaji wa watalii wanaofika wilayani humo kupitia kampuni ya Rungwe Tea and Tours , watalii wengi wanafika na kukiri kwamba daraja hilo ni kubwa zaidi kuliko madaraja mengine ya asili yaliyopo duniani.
Suleiman anasema Daraja la Mungu linatembelewa na wazungu wengi kutoka nje kupitia kampuni  anayofanyia kazi lakini pia wapo wanafika wenyewe.
Ukitaka kwenda darajani hapo, ukitokea jijini Mbeya utapita barabara kuu ya Mbeya kwenda Kyela na  utateremkia Kijiji cha Kyimo maarufu kwa jina la ‘KK’ ambapo utapata usafiri wa pikipiki au magari ya kukodi  kukupeleka kwenye shimo la Mto Kiwira umbali wa kilometa karibu 10 kutoka barabara kuu.
Katika safari ya kwenda huko utaiona Sekondari ya Iponjola na  baada ya hapo utaingia Kijiji cha Lugombo na kuikuta Sekondari ya mchepuo wa Kiingereza ya God’s Bridge International School ambayo imeanzishwa miaka mitatu iliyopita ikiwa na jina hilo ili kuenzi  Daraja la Mungu.
Safari itaendelea ukijionea pia Shule ya Msingi Kibwe na hatimaye ofisi ya Kijiji cha Lugombo kabla ya kuanza mteremko mkali ambao barabara imewekewa lami ili kupunguza madhara kwa vyombo vya usafiri hadi mtoni
Ukianza kuukaribia mto, utaona  kwa ng’ambo majengo mengi mazuri yaliyotuama umbali wa kilometa moja chini ya miti pembezoni  mwa  Mto Kiwira. 
Majengo hayo ni ya Chuo cha Askari Magereza  Tanzania .Kwa asilimia kubwa majengo ya chuo hicho yapo pembezoni ya Mto Kiwira , lakini kabla ya kuuvuka mto kupitia daraja lillilojengwa na Serikali  utapinda kushoto kuekelea kwenye Daraja la Mungu.
Baada ya mita 400 hivi utalikuta daraja lingine ambalo linaelezwa kwamba lilijengwa na Warusi waliopewa kazi ya kujenga mtambo wa kufua umeme kwenye maji yaendayo kasi karibu na Daraja la Mungu.
Ukiwa kwenye daraja hilo utaliona Daraja la Mungu likiwa kusini mwa mto ambalo limeundwa kwa umaridadi wa aina yake.
Daraja hilo kwa chini limejikunja kama upinde, lakini juu kukiwa na nafasi yenye upana unaotofautiana, kwani lipo eneo lenye upana wa mita tano na mita mbili. Kwa kweli ni la ajabu kwani hata maji yanavyokatisha eneo hilo yanatisha.
Kutisha kwake kunatokana na maji hayo, badala ya kunyoka kulikatisha daraja, yanaelekea kwanza kwenye mwamba uliopo mashariki na kuzunguka kuelekea kaskazini na hatimaye kuelekea kusini yakiwa na kasi ndogo chini ya daraja hilo kabla ya kupokewa tena na poroko lenye kasi linalotoa mvuke wakati wote.
Penye poromoko la maji hayo panaelezwa kwamba Serikali iliwatafuta Warusi ili wasaidie kuweka mitambo ya kufua umeme mwaka 1969 hafi 1978 walipofukuzwa kwa saa 24 bila kufanikisha suala hilo.
Uvumbuzi  wa Daraja Mungu
Ni wazi daraja hilo ni la asili kutokana na miamba ya Mwenyezi Mungu kuunganishwa na kuruhusu maji kupita chini yake. Lakini ni nani aliyegundua daraja hilo?
Swali hili ni vigumu kujibiwa, lakini kutokana na historia iliyotolewa na watu waliotangulia eneo hilo ni kwamba wagunduzi wa kwanza walikuwa nyani.
Lusajo Mbwiga (30) ni mjukuu wa aliyekuwa kiongozi wa mila wa eneo hilo aliyekuwa akiitwa Mwahesya.
Kijana huyo ndiye aliyechiwa mikoba yote ya uchifu  na hatimaye  wanakijiji wa Mboyo kumridhia  kwa ujasiri wake katika kutambua mazingara na vituko vya Mto Kiwira.
Mbwiga ambaye kwa sasa anajulikana zaidi kwa jina la Chifu,  anaamini kwamba Mto Kiwira unaongoza kwa kuua watu na anasema ndiye aliyebeba mikoba ya kuzama kwenye mto huo kuopoa maiti yoyote inayopotea. Anasema kwa maelezo ya babu yake ni kwamba Daraja la Mungu liligunduliwa na nyani.
‘’Baada ya nyani kupita waliofuata nyayo za nyani walikuwa watu wa kabila la Waandali kutoka Wilaya ya Ileje  ambao awali walikuwa wakivuka mto huo kwa kuruka eneo lililoaminika kuwa na maajabu na kuua watu wengi.
Eneo hilo linatajwa kuua  Waandali wengi kwa kutumbukia , lakini wachache walifanikiwa kuruka.“Wachache walioruka waliamini kwamba waliotumbukia hawakuruka kwa ujanja’’ alisema na kuongeza kwamba ndio maana hapa panaitwa ‘’atanyerite bukomu’ ikiwa na maana kwamba  hakuruka vizuri ndio maana ametumbukia kwenye mto.
Kwa mujibu wa Mbwiga Waandali hao  walikuwa wakitoka Ileje huko Magharibi ya mto wakielekea Rungwe Mashariki na walipofika hapo kiongozi wao aliruka akiwa na mnyama mbuzi aliyemfunga mgongoni, lakini waliofuata walipojaribu kuruka walianza kutumbukia na kufa.
Eneo hilo ambalo pia ni la maajabu ya Mto Kiwira lipo mita 800 kaskazini mwa Daraja la Mungu ambapo pia  limejengwa daraja ambalo sasa linatumika kwa watu na vyombo vya usafiri kuunganisha Wilaya za Rungwe na Ileje.
Naye Mzee Brown Mwapulo (76) ambaye ni kiongozi wa kimila Kitongoji cha Ibaga kwenye Kijiji ch Lugombo anasema miaka ya 1930 hadi 1950 Waandali wengi walitumbukia eneo hilo na baada ya kuona hivyo walianza kutafuta eneo lingine la kuvuka na hatimaye waliwaona nyani wakivuka eneo la Daraja la Mungu  na kuamua kuwafuata.
 "Baada ya watu hao kuliona daraja hilo, ikawa mwanzo wa kutumika na limekuwa likitumia hadi walipokuja Warusi na kujenga daraja lingine karibu na eneo hilo’’ anasema.
Hali ya Daraja la Mungu kwa sasa
Mwangalizi  wa daraja hilo, Mbwiga anasema Daraja la Mungu limeanza kupata misukosuko kutokana na mto kuendelea kuchimba zaidi mwamba ambao kwa sasa unabomoka upande wa magharibi.
 Pia anasema miti mikubwa imeota juu ya daraja na kusababisha mizizi inayopasua mawe  na hatimaye  yanayodondoka.
“Kwa ujumla “matunzo ya kivutio hiki  bado hayajapewa kipaumbele’’ anasema.
Hata hivyo anadokeza kwamba uongozi wa Wilaya ya Rungwe umeshatamka kuboresha eneo la Daraja la Mungu na kwamba tayari umetoa kitabu cha risiti ili kuwatoza watalii wanaotembelea eneo hilo.
“Wanafunzi wanaotembelea ni bure, lakini watalii kutoka nje ya nchi wanatakiwa kulipa walau Dola 2 za Marekani ambazo ni sawa na Sh 5,000.
Mkakati wa Serikali ya Wilaya Rungwe
Mkuu wa wilaya hiyo, Chrispine Meela anasema  Daraja la Mungu ni moja ya vitutio vingi vya utalii wilayani humo.
Meela anasema Serikali imeamua kuyaweka wazi maeneo yote ya utalii yakiwamo ya Mto Kiwira naq maajabu yake.
“Januari 18, mwaka huu, tuliunda kamati ya wadau 15 wa sekta ya utalii ambayo itaandaa uzinduzi maalumu wa kutangaza vivutio vya utalii wilayani humo’’anasema.
Meela anasema kamati hiyo imeshirikisha wadau mbalimbali wakiwamo wenye hoteli, kampuni za kusafirisha watalii, na wananchi baada ya kugundua wilaya ikiwa na vivuti vingi vizuri vya utalii.

Anataja baadhi ya vivutio kuwa ni Daraja la Mungu, Ziwa Ngozi, Ziwa Kisiba, Boma la Wajerumani Masoko, Maporomoko ya Kaporogwe, Maporomoko ya Mto Suma kwenye Kijiji cha Malamba na Mlima Rungwe ambao ni wa tatu kwa urefu baada ya Kilimanjaro na Meru nchini.
 
Top